Mtu anasema kuwa ana mpenzi wake ambaye wanapendana sana lakini sasa hivi hamuelewi baada ya kuona upendo umepungua. 
Ukiangalia  kichwa cha habari hapo juu, kina jibu la moja kwa moja lakini ni vigumu  mtu kuelewa kwa vile bado hajifahamu katika mapenzi amesimama upande  gani.
Unasema wewe na mpenzi wako mnapendana sana, lakini sasa hivi  mpenzi wako humuelewi, ukimpigia simu hapokei kama zamani au akipokea,  anakuwa na majibu ya mkato tofauti na mwanzo wa mapenzi yenu.
Hili  swali naweza kusema limekuwa fasheni katika mapenzi ya sasa, hasa kwa  wapenzi waliokuwa pamoja na baadaye kutengana kwa ajili ya kazi au  masomo, kwa hawa lazima baada ya muda tatizo hili hutokea.
Kuna nini?
Wengi  sehemu hii huwashinda kwa vile huwa na mapenzi ya mdomoni na machoni.  Wapenzi wengi huwa na heshima na uaminifu kama wanawaona wapenzi wao  kila siku, mtu huogopa kufanya usaliti kwa kuwa mpenzi wake yupo, lakini  huyohuyo huwa hana uaminifu anapokuwa peke yake sehemu ya mbali.
Huwa mwepesi kuanzisha uhusiano mpya kwa kuamini ni wa kupita.
Kwa  vile wengi hawana mioyo migumu ya uvumilivu, hujikuta wakizama moja kwa  moja na kuwasahau waliowaacha nyumbani. Hapo ndipo ule utata unaosumbua  huanza. Utasikia nipo bize au simu kutopokelewa kabisa na kwa wengine  huwapa wapenzi wao wapya wapokee.
Kwa vile uliye mbali na mpenzi wako  hujui mwenzako kazama kwenye penzi jipya, hapo ndipo huanza kuumia  moyoni ukiamini kabisa mpenzi wako anakupenda lakini hujui tatizo.
Kama  ungekuwa mfuatiliaji mzuri wa makala zangu, ungejua mtu mwenye mapenzi  ya kweli yupo vipi. Mwenye mapenzi ya kweli ni tulizo la mawazo ya  mpenzi wake, ni mpole na mwenye huruma na mara zote hujiepusha kuwa  sehemu ya maumivu yako.
Hivyo, ukiona mpenzi wako haeleweki,  unatakiwa kuanza kuizoea hali ile ili kujiandaa kwa penzi jipya, kwa  vile ule mche wa mapenzi ulioupanda ndani ya moyo wa mwenzako umesinyaa.
Usipende  kujitesa kwa kujitakia, kama umeona kabisa kuna mabadiliko ndani ya  penzi ni wakati wa kuchukua uamuzi mgumu ili kunusuru mateso yasiyo na  sababu.
Jiepushe kuishi mapenzi ya mazoea kwa kuamini unapendwa  wakati unateswa, hakuna upendo wa mateso hata siku moja. Mapenzi ni  furaha na wala si karaha. Acha kuusemea moyo wa mwenzako kuwa anakupenda  wakati ndiye chanzo cha ugonjwa wako wa moyo.
Kabla ya kuchukua  uamuzi mgumu wa kuvunja penzi, msomee mpenzi wako mashtaka na kumueleza  ukweli kuwa umechoka kuumia, akikosa utetezi unaoeleweka, una nafasi ya  kuvunja penzi. 
Kama atakuwa tayari kukiri makosa na kujirudi,  unaweza kumpa nafasi nyingine lakini akirudia makosa, achana naye,  fungua ukurasa mpya.
Saturday, March 17, 2012
Anakupenda lakini anakutesa, mapenzi yapo wapi
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment