Naendelea kuchambua mada yetu tuliyoianza wiki iliyopita na sasa nahitimisha na dalili nyingine zilizosalia. Twende pamoja...
KUSITA KATIKA MAAMUZI
Kipengele  hiki hakiko mbali sana na kilichotangulia lakini kuna baadhi ya vitu  katika kuelekezana. Kwamba unakuta mtu ana vitu vingi sana kichwani  mwake lakini hawezi kuchukua hatua kuvikamilisha na kuviweka katika hali  ya utendaji.
Hapa nazungumzia suala la kusita katika kuchukua hatua  juu ya unachokiwaza na kukifikiria maishani. Mfano labda mtu yuko  kijijini, ana kipaji cha kuandika habari au ana ndoto za kuwa  mfanyabiashara, ameamua kwenda mjini kutafuta hizo njia za kumuwezesha  kutimiza ndoto yake. Tatizo linakuja katika kuchukua hatua za  utekelezaji juu ya jambo hilo. Anakuwa hajiamini kama anaweza kukaa  mbali na nyumbani kwao. Anakuwa mtu wa kusita katika kufanya maamuzi  sahihi.
Wakati mwingine una rafiki ambaye hakika hana faida yoyote  kwako, yeye ni mtu wa kukunyonya tu lakini hana mchango wowote kwako.  Sasa unashindwa kufanya maamuzi sahihi ya kuachana naye kwa kuhofia kuwa  bila yeye utapwaya. Eti umemzoea sana. Huku ni kusita katika maamuzi  ambapo nasema ni dalili ya kutojiamini. Usisite, chukua uamuzi muafaka  tena kwa wakati. Jiamini katika kuamua mambo.
KUJIKOSOA
Hii ni  dalili kubwa sana ya kutojiamini maishani. Unakuwa ni mtu wa  kujifananisha na wengine kisha kujishusha katika thamani. Hapa  nazungumzia watu walio na mawazo mazuri sana lakini kabla  hujayawasilisha kwa watu, unaanza kujikosoa. Hivi kweli hili ni jambo  jema kulisema? Au nitaelewekaje? Watakubali kweli mawazo yangu? Yaani ni  mtu wa kujikosoa kila wakati, kuona kama huna kitu cha kusema au  kuwasilisha kwa wengine.
Achana na tabia ya kujilinganisha na  wengine. Iwe kwa mavazi, fedha, uzuri wa sura nk. Jione kuwa wewe ni  bora kuliko wengine kama yeye ni mzuri wa sura, basi ni yeye. Kama ana  nguo nyingi kuliko wewe sawa. Lakini jambo la msingi hapa ni kujiamini  na kuondoa zana ya kujikosoa. Mchango wako ni mkubwa sana katika jamii .  Ni suala la wewe kujiamini. Jiamini kuanzia leo.
WIVU
Hapa  nazungumzia wivu ambao hauna maana hata kidogo. Utakuta mtu anampinga  mtu pasipokuwa na sababu maalum. Unakuwa mtu wa kuwapinga wengine kila  wakitaka kufanya jambo muhimu la kimaendeleo kwa kuhofia tu kuwa  watakuzidi kwa sababu hujiamini katika utendaji wako wa mambo.
Unakuwa  unawaza, f’lani akifanya hivi atanizidi katika suala hili, au akifanya  hiki mimi nitaonekana sifai mbele za watu na jamii kwa ujumla. Ni mtu wa  kuwaza uwezo wa watu pasipo kujifikiria mwenyewe. Achana na wivu wa  kutojiamini. Jiamini sasa. Kwa kufanya hivyo kila kitu kitanyooka na  maisha utayaona yapo tofauti.
MUHIMU
Maisha yanaendelea kama  kawaida,  jitahidi kuondoa zana zote potofu katika maisha, ondoa fikra  za kushindwa hata kidogo kani wewe hukuumbwa kuja kuteseka hapa chini ya  jua.
Thursday, March 15, 2012
Dalili 5 za Mtu asiyejiamini II
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment