Thursday, March 15, 2012

Anza Mwaka na Mawazo Mapya II

UNAPO tafuta mafanikio ni lazima kwanza upitie shida na vikwazo vya kila namna.
Hakuna mafanikio ya bure, ni lazima uyatolee sadaka. Sadaka ya jasho. Ni lazima ufanye kazi kwa nguvu na maarifa ya hali ya juu.

Mateso ya maisha ni makali sana, tena wakati mwingine Mungu huzidisha ukali kwa lengo la kutaka kuona kama ukipewa hiyo neema utailinda.

Siri nyingine ambayo nataka kuiweka wazi leo ni kuwa, vikwazo vipo katika safari ya kusaka mafanikio.
Ni lazima ulie kwanza ili baadaye ufaidi mema ya nchi! Usivichukie vikwazo vya maisha kwani vinakomaza, vigeuze kama kuni za kuchochea hamu yako ya kufanikiwa.

Maisha ya dhiki unayoishi si yale ambayo yalimaanishwa kwako, badala yake maisha ya kweli yanakuja.
Lakini yatakuja endapo utafanya kazi kwa nguvu, bidii na kumfanya Mungu ndiye nguzo muhimu maishani mwako. Nilishawahi kusema huko nyuma kuwa, kuna wakati maisha huonekana magumu sana.

ZINGATIA HAYA:
Sasa mateso yote yamefika kikomo, naomba uyazingatie kwa makini nitakayo yaainisha hapa. Yatabadili maisha yako. Mafanikio yako unayo mkononi mwako ni uamuzi tu. Ndani yako kuna uwezo mkubwa mno ambao hakika hujaamua kuutumia ipasavyo.
Hujataka kuitumia vizuri zawadi amabayo Mungu alikupa. Zawadi ya akili.
Hukuumbwa kabisa uje uhangaike kama ulivyo sasa. Ukiamua kubadilika ni mara moja tu. Acha kulia, futa machozi.
Muda wa kufaidi matunda ya dunia umewadia kama utazingatia vizuri ninayoandika hapa.
Umeteseka kwa muda mrefu mno, miaka yote imekuwa michungu kwako, machozi yamekuwa faraja yako namba moja!.
Mwaka huu wa 2012 ni mwaka wa mapinduzi kwako. Ndiyo! Ni mwaka ambao hakika utakupa thamani ya utu wako. Amini hilo.
Kwanza kabisa, tumia muda mwingi kuwa peke yako katika sehemu ambayo imetulia, hakikisha hakuna kelele aina yoyote katika eneo hilo.
Chukua kioo kisha kiweke mbele yako. Jiangalie kwa muda wa dakika zisizopungua kumi kisha sema maneno haya.
“ Mungu baba, ahsante kwa kuniumba hivi nilivyo, nakushukuru kwa kila hatua uliyonipitisha maishani mwangu tangu nazaliwa hadi sasa. Nakushukuru kwa kunipa zawadi hii ya pekee, zawadi ya akili ambayo sijaitumia hata theluthi yake. Sasa nimeamua kuwa uliyenimaanisha.
Kuanzia leo nayabadili maisha yangu kwani nimechoka kukaa hivi”.
Baada ya kusema hayo, sasa amini kuwa umekuwa huru.
Haijalishi kwa una miaka mingapi, lakini chukulia kuwa mateso yote ya huko nyuma ni kama historia ambayo kamwe haiwezi kujirudia na uisahau kabisa.
Anza kubadili fikira zako kwa kuamini kuwa hukuumbwa kushindwa kabisa. Kaa chini ufikirie ni kitu gani ambacho ukikifanya kinaweza kubadili maisha yako kabisa.
Jichunguze kwa makini, hakikisha unapata wazo la biashara. Katika maisha kuna vitu vitatu muhimu sana ambavyo ni wazo, watu na fedha.
Kamwe vitu hivyo haviji kwa pamoja. Pata kwanza wazo ndipo mengine yafuate.
Naomba nikukumbushe kuwa, ukianza safari yako ya kutafuta maisha, yatainuka mabango mengi kutoka kwa watu ambao mimi huwaita Negativism (wavunja moyo) ambao kazi yao kubwa ni kuvunja wenzao moyo. Watasema huwezi kwa sababu tu hukusoma, kwenu masikini, baba yako hakuweza.
Nataka nikuambie kuwa, hata kama watasema nini juu yako, maneno yao yasikuvunje moyo hata kidogo kwani wao si waamuzi wa maisha yako. Mwalimu wa somo la ujasiriamali, Eric Shigongo aliwahi kusema kuwa; ‘Someone’s opinions over you does not have to be your reality’(mawazo ya mtu juu yako yasiwe ukweli wako).
Maadui huongezeka mara dufu unapotafuta mafanikio, kwani wengi huwa hatupendi kuona mtu anapiga hatua ya maendeleo maishani.
Kwa hiyo basi acha wakudharau lakini ukifumba macho na kuzidi kusonga mbele, ipo siku wanaokudharau watakusalimia kwa heshima huku wengine wakihitaji msaada wako.
Itaendelea wiki ijayo.

Related Posts by Categories



No comments:

Post a Comment