“MIMI ni masikini, sijasoma, maisha yanazidi kuwa magumu kila kukicha.  Nawalaumu wazazi wangu kutonipeleka shule.” Hii ni kauli ya mama mmoja  ambaye alikuja ofisini kwangu kuomba ushauri.
Japo alikuja analia,  mwenye huzuni na simanzi kwa jinsi maisha yalivyokuwa yanamuendea,  namshukuru Mungu aliondoka huku uso ukiwa na tabasamu.
Watu wengi  bado wamegubikwa na fikra kuwa bila elimu ya darasani huwezi kufanya  chochote maishani na ili uwe na maisha bora ni lazima uende shule.
Ndiyo  maana utakuta wazazi wengi wanawaambia watoto wao kuwa nendeni mkasome  ili muwe na maisha bora. Kauli hii huota mizizi akilini mwa watoto  lakini wanapoanza kuukabili ulimwengu halisi, ndipo mambo hubadilika  kabisa.
Nataka kuweka kumbukumbu sawa kuwa, kusoma si kitu na  kutokusoma bado si kitu, bali ili ufanikiwe maishani inategemea na jinsi  unavyotenda mambo.
Kuna msemo mmoja wa kizungu ambao napenda sana kuutumia unaosema ;
‘Life can compel you to move either foward or backward depending on what you do.’
(Maisha yanaweza kukupeleka mbele au nyuma kutegemea na jinsi unavyofanya). Hapa hakuna kusoma wala kutosoma.
Binafsi naamini sana katika elimu ya darasani, tena nahamasisha watu kwenda shule ili wapate mwanga wa maisha.
Ndugu  zangu, mafanikio maishani ni uchaguzi wa mtu mwenyewe, kufanya kazi kwa  nguvu na kutumia vyema kila fursa inayopatikana. Ukiangalia maghorofa  yaliyopo Kariakoo na kwingine, utashangaa utakapooneshwa wanaoyamiliki.  Wengi wao hawajasoma hata kidogo lakini wameweza kufikia kiwango hicho.
Nilishasema  huko nyuma kuwa siri kubwa ya kufanikiwa maishani ni kujibidisha katika  utendaji wa kazi huku ukiwa na nidhamu na matumizi ya fedha, watu muda  na kuendelea kuwa na miradi mbalimbali.
Elimu ya mitaani ambayo mimi  huiita Street University ni muhimu kuliko ile ya darasani. Hata kama  umesoma hadi vyuo vyote duniani lakini ni lazima uje mtaani ujifunze  maisha yanavyotakiwa kuendeshwa. Mara nyingi tunayofundishwa darasani ni  tofauti kabisa na tunayokutana nayo katika maisha halisi.
Nataka kukuhakikishia kuwa hata kama hujasoma sana, mafanikio katika maisha ni uamuzi.
Kuna makundi matatu ya elimu ambayo yanajitegemea.
Kundi  la kwanza ni Elimu ya Kitaaluma (Academic Education), Elimu ya Chambuzi  (Proffesional Education) na Elimu ya Fedha (Financial Education).
Zote  hizi ni muhimu sana lakini elimu ya fedha naipa kipaumbele cha kwanza  kutokana na ukweli kuwa ni lazima ujue jinsi gani unatakiwa kuzitumia  fedha zako hata kama ni ndogo au nyingi kiasi gani.
Elimu ya fedha  inapatikana shuleni na mtaani lakini tofauti ni kuwa, shuleni utaipata  elimu hii kwa nadharia lakini mtaani utaipata kwa vitendo. Ukienda  kinyume na utaratibu huo, kufanikiwa katika maisha yako itakuwa ndoto.
Napenda  kuhitimisha kwa kusema kuwa safari ya mafanikio maishani inahitaji  uvumilivu na kujitoa kwa dhati na ni lazima uumie, uvuje jasho,  uhangaike ndipo mambo yaweze kwenda sawa.
Tuache kupandikiza  mbegu mbaya kwa watoto wetu kuwa waende shule ili waajiriwe ili wawe na  maisha bora, badala yake tuwaambie ukweli kuwa unaweza kusoma na bado  usiwe na maisha bora isipokuwa ili uwe na maisha bora ni lazima ufanye  kazi kwa nguvu na kuzifanyia kazi kila fursa unazopata. Tuwaambie kuwa  tunaenda shule ili kupanua uelewa na si kufanikiwa maishani.
Uwezo wa kufanikiwa uko mikononi mwako, ni wewe tu kuamua.
Thursday, March 15, 2012
Elimu ya Darasani Si Kila Kitu
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment