Watafiti  kutoka Chuo Kikuu cha British Columbia (UBC),  wanasaidia majibu ya swali hili kulingana na uchunguzi walioufanya na  kuuchapisha katika Jarida la ‘Journal Science’ la Machi 21, 2008 kwamba  watu wengi hutumia fedha zao kununua furaha.
Inaelezwa katika  ripoti zao kwamba watu wengi wanapokuwa na fedha hupenda kuzitumia kwa  kununua kadi, zawadi kwa wawapendao, kukusanyika pamoja na marafiki ili  kushiriki furaha za pamoja kwa kunywa, kula na kustarehe sehemu  mbalimbali.
“Ni ukweli ulio wazi kwamba fedha nyingi hutumika  kununua furaha.  Tumeona hili katika uchunguzi wetu uliohusisha zaidi ya  watu 630 kutoka nchini Marekani ambapo asilimia 87 kati ya  tuliowadodosa kuhusu matumizi ya fedha zao walisema wanazitumia  kununulia mahitaji na vitu vidogovidodo zikiwemo zawadi na nguo, ”  anasema Profesa Elizabeth Dunn mmoja wa watafiti wa UBC.
Utafiti  huo wa kitaalamu una maana kubwa katika maisha ya binadamu hasa  linapokuja suala la mafanikio. Ukiangalia kwa makini, watu wengi hutumia  fedha kuleta furaha katika maisha yao, jambo ambalo ni hatari  kimaendeleo.
Uhusiano wa matumizi ya fedha, tabia za mwanadamu na  kanuni za mafanikio ni mambo yanayohitaji elimu ili kumfanya mtu  atambue hasara za ununuzi wa furaha ambazo anazipata pale anapotoa fedha  zake kujipatia vitu anavyovipenda.
Ni mambo yaliyo wazi kwamba, mtu  anaponunua pombe au kuandaa pati ya kuzaliwa kwake, hufurahi, lakini  kanuni za maendeleo haziko kwenye msingi wa furaha ya kununua kwa siku  moja bali matarajio ya furaha.
Katika hali ya kawaida, wengi  hawataki kutarajia furaha bali kufurahi kila wanapohitaji. Ili kujua  zaidi kuhusu hali hii, ni vema tukajiuliza ni nani aliyepata kujenga  nyumba huku akifurahi? Tunasikia kila siku watu wakisema, “Jamaa amekuwa  bahili sana, sijui anajenga nyumba?” au “Maisha yangu yamekuwa magumu  sana siku hizi namalizia kibanda changu.”
Tafsiri ya kumalizia  kibanda ni maisha magumu na ubahili, lakini baada ya nyumba kukamilika  kile kinachotajwa kama furaha ya mafanikio hujitokeza na kumfanya  mhusika kujua kuwa kipindi cha ubahili kilikuwa ni cha furaha pia,  tofauti na mtazamo wa wengi.
Watu huniuliza; kwa nini fedha zangu  hazikai,  yaani kila nikizipata zinakwisha hivihivi wala sijui hata  nimezifanyia nini?  Waulizao maswali ya namna hii huwa hawajui kuwa  maisha yao wameyaelekeza katika kununua furaha.
Wengi wetu  tumekuwa  wepesi kutii tamaa kwa kununua mavazi, kwenda saluni, kula  vyakula vinono, kufanya starehe na kusahau kufanya mambo ya msingi ya  kujijengea uwezo wa kutufikisha kwenye furaha ya muda mrefu yaani kuishi  maisha yenye mafanikio makubwa.
Bila shaka kila anayetaka  kufanikiwa lazima aache kuwa mteja wa furaha, azuie fedha zake zisitoke  kwa lengo la kuufurahisha mwili, kujenga urafiki na watu wengine na  kujikweza.
Mtu yeyote akitaka kujua kama anaishi kwa kununua  furaha achukue kalamu na karatasi, aorodheshe matumizi yake kwa mwezi  atagundua asilimia zaidi ya 85 ya mshahara wake, kama walivyosema  watafiti wa UBC, zimetumika kununulia furaha.
Katika orodha hiyo  atakuta amewapa ofa watu fulani, alimhonga msichana, alilipia kiingilio  cha muziki, alilipa pango kwenye nyumba ya kulala wageni, alinunua  pombe, yote hayo ni mambo ya fedha kununua furaha.
Nimalize kwa  kusema kwamba, makala haya yanashauri kila mtu awe tayari kuishi kwa  kutegemea furaha si kununua furaha kwa sababu ni hasara kufanya hivyo.
Bila  shaka wanaotegemea furaha wataweka benki fedha zao ili waanzishie  miradi, watanunua mifuko ya simenti, watasomesha watoto wao, watanunua  viwanja na kadhalika, mambo ambayo ukiyatazama kwa juujuu utadhani  yanapunguza uwezo fulani kwenye maisha lakini kumbe ndiyo mafanikio  yenyewe.
Saturday, March 17, 2012
Je Ni Kweli Fedha Hununua Furaha
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment