Familia nyingi na hasa watoto wamekuwa wakikatazwa na wazazi wao  kuangalia sinema kwa fikra kwamba zinapumbaza na kupoteza muda, jambo  ambalo wanasaikolojia wanapingana nalo.
Mwanasaikolojia Dorothy  Halla-Poe kutoka Marekani anabainisha kitu tofauti na mtazamo wa wengi  kuwa, kazi ya filamu si burudani pekee, bali tafiti zinaonyesha kuwa ni  njia yenye mafanikio makubwa katika kujifunza mambo na kutibu baadhi ya  matatizo yanayowakabili wanadamu.
Eti, tuamini kwamba sinema  zinafundisha na kutatua shida zetu? Jibu ni ndiyo kwa asilimia mia moja,  kwani ndani ya filamu uanadamu wetu unakamilishwa kwa kujifunza kupitia  kusikia, kuhisi na kutafakari, mambo ambayo yanapatikana ndani ya  filamu.
Hakuna ubishi kwamba uchaguzi wa simulizi, visa na tungo  zinazopatikana kwenye filamu ndiyo jambo pekee linalohitajika  kuzingatiwa, hii ikiwa na maana kwamba kujifunza, kujitibu matatizo yetu  kunaanzia kwenye kile tunachotaka kukitazama ndani ya filamu.
Upo  ushahidi wa kutosha juu ya watu wenye matatizo ya hisia za kimapenzi  kumaliza ugonjwa wao kwa kutazama sinema za ngono huku wengine wakitajwa  kujengwa kiimani, ujasiri na uvumilivu kupitia michezo ya kuigiza.
Kwa  msingi huo hatuwezi kupuuza  utazamaji wa sinema kwani inawezekana   kuihamasisha jamii yetu kuwa hodari katika mambo wanayoyaona yakitendwa  na waigizaji.
Kupitia filamu tunaweza kuwapatia watoto wetu moyo  wa kishujaa mithili ya michezo inayoigizwa na wasanii. “Mimi Rambo”  “Basi mimi Schwarzenegger” Naamini tumeshasikia watoto wakijifu kupitia  majina hayo ya wacheza filamu.
Hii ina maana kwamba, filamu za  waigizaji hao zimesaidia kwa kiwango kikubwa kuwajenga watoto katika  ujasiri unaoweza kuwa mfano mmoja tu wenye faida na motisha unaopatika  kwenye filamu na hivyo kutia nguvu mada hii kwamba, tunaweza  kuwahamasisha vijana wanaochipukia kuwa akina Rais Julius Nyerere, Kwame  Nkrumah, Nelson Mandela kwa kuwapatia filamu za viongozi hao na  kuzitazama.
Kama hilo halitoshi wanasaikolojia wanaamini kwamba,  mtu anaweza kujitibu mwenyewe tatizo la msongo wa mawazo kwa kuangalia  filamu zenye ujumbe unaohusiana na tatizo lake na hivyo kujiongezea moyo  wa ushindi kupitia waigizaji anaowataza kwenye sinema.
Kwa  mfano, mtu anaweza kuwa mgonjwa miaka sita na akawa katika hali ya  kutaka tamaa lakini akiletewa filamu inayomuonyesha mtu mwenye ugonjwa  kama wake akihangaika na hatimaye kupona hata yeye atafarijika na  kuamini kuwa ipo siku atapona kama yule muigizaji na hivyo kupata imani  ambayo itamsaidia kuishi.
Ninachotaka kueleza hapa ni kwamba ,  filamu hutengeza ndoto za maisha, huleta ubunifu na kuamsha hamasa ya  kufikia malengo yetu, hivyo si busara kuipuuza tasnia ya uigizaji kwa  mtazamo kuwa inawapotezea watu muda wa kutafuta mafanikio.
Jambo  muhimu la kuzingatia kama nilivyodokeza hapo mwanzo ni kuwa makini na  uchaguzi wa filamu tunazotaka kuziangalia. Maana hakuna ubishi kwenye  elimu hii kwamba mtoto akizoezwa kuangalia filamu za kikatili  atabadilika na kuiga tabia ya ugomvi, vivyo hivyo wanaopendelea sinema  za ngono zitawashawishi kufanya kitendo hicho lakini sinema za  kuelemisha ni msaada mkubwa wa kukuza ufahamu wa watu.
Naamini,  wazazi wengi wakitumia filamu zinazoonyesha mateso wanayopata watoto wa  kike baada ya kupewa mimba wakiwa shuleni na baadaye kutengwa na familia  zao wanaweza kufikisha ujumbe wenye nguvu kwa watoto wao wa kike zaidi  ya wao kutumia ukali na vitisho.
Ukweli ni kwamba, filamu zina  uwezo mkubwa wa kutengeneza hisia kama nilivyosema kuliko maneno ya moja  kwa moja, ndiyo maana upo utofauti mkubwa kati ya ujumbe unaotumwa kwa  njia ya wimbo na ule unaoweza kutolewa kwa njia ya sinema.
Kama  hilo halitoshi, kusahau maneno ni rahisi zaidi kuliko sinema hivyo   kutumia njia ya filamu kufundishia kunatajwa kuwa ni njia bora zaidi ya  kutolea maelekezo hasa kwa watoto ambao kusahau ni jambo jepesi kwao.
Saturday, March 17, 2012
Utafiti:Utazamaji filamu ni tiba ya matatizo
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment