Saturday, March 17, 2012

Kanuni za Kuishi na Wanaokuchukia

Maisha ya mwanadamu wakati mwingine yamejaa matukio ambayo mwenyewe hawezi kuyaepuka. Moja kati ya hayo ni mtu kuchukiwa na wenzake na kujikuta katika wakati mgumu iwe kwenye familia na hata kazini.

Mara nyingi uamuzi mwepesi ambao wanaochukiwa huwa wanauchukua ni kujibu mashambulizi huku wengine wakiamua kujiepusha eti kwa kuhama maeneo wanayoishi au kujitenga na wenye chuki.


Njia hizo zinaweza kuwa sahihi lakini si zenye kuleta mafanikio ya kudumu. Ni vema ikafahamika kwamba kujibu mapigo ya chuki hukuza migogoro na jambo baya zaidi ni kwamba maadui huongezeka.


Pengine msomaji wangu ungependa kujua kwa nini maadui huongezeka? Jibu ni kwamba wanaompenda huyo unayemlipiza kisasi wataingilia ugomvi na kufanya kila liwezekanalo wakumalize.


Nimewahi kushuhudia watu wawili kazini wanahitilafiana kwa jambo fulani lakini mwisho kundi la wafanyakazi liliingia kwenye mgogoro, chanzo kikiwa ni kile kile cha watu wawili wa mwanzo.


Kwa nini hali hiyo hutokea? Kwa sababu ya utashi wa kibinadamu na msukumo asili wa kupenda kwani sote tunajua hata wezi hupendana na kuteteana.


Aidha, tunapotazama uamuzi mwingine wa kukimbia maadui zetu tunajikuta tukipata utata wa kimaamuzi kwa sababu hatuwezi kuwakimbia wote kwenye maisha yetu, tukifanya hivyo tutakuwa watu wa kuhamahama kila siku, maana wenye chuki ni wengi na wanaanzia kwenye familia zetu mpaka kazini.


Jambo la msingi la kufanya pale tunapobaini kuwa kuna watu wanaotuchukia mahali popote pale, ni kutumia njia zifuatazo;

KWANZA: Ni kufunua ukweli kuhusu kuchukiwa, yaani tuwaambie wanaotuchukia kuwa hatufurahishwi na chuki, tuwaombe msamaha ikibidi.

PILI: Tujilinde wenyewe kwa kupunguza uhusiano na mwingiliano wa kimatendo na kauli hasa zenye kupingana.

TATU: Tutumie muda mwingi sana kuambatana na wanaotupenda na kupata faraja kwao, lengo ni kuharibu hisia mbaya zitakazokuwepo kwenye akili zetu juu ya wanaotuchukia.

NNE: Tusiachie nafasi za kimaisha wazitawale adui zetu; “mimi sitafanya kazi na fulani acha afanye yeye aone raha.”

“Nitaacha kazi ili tusigombane naye zaidi.” Kamwe tusitoe nafasi za utawala badala yake tuonyeshe wengine kwamba tunatekeleza majukumu yetu ya kimaisha vizuri ingawa tunachukiwa kwenye familia au kazini.

TANO: Tuwashirikishe ndugu/rafiki wenye busara katika kila kwazo ili wasaidie namna ya kufanya. Tusichukue uamuzi wenyewe bila ushauri hasa tunapokuwa na hasira. Tujipe muda wa kutafakari zaidi kila jambo la chuki tunalofanyiwa kabla ya kuamua kufanya chochote.

MUHIMU: Tuepuke kukuza mgogoro kwa kuwajumuisha wengine kwenye ugomvi. Tusikumbatie tatizo na kulikuza kwenye mawazo yetu. Tuwe watu wa kupuuza na kupunguza msongo wa mawazo.

Tusimwambie kila mtu tatizo letu. Tusimame kwenye nguzo ya uvumilivu kwa muda mrefu kabla ya kukata tamaa.

Related Posts by Categories



No comments:

Post a Comment