NI wiki nyingine tena tunakutana kupitia safu hii nikiamini muwazima na  mlikuwa na wakati mzuri sasa katika kusherehekea Siku ya Wapendanao.
Sitaki  kufikiria jinsi ‘mlivyoinjoi’ siku hiyo lakini naamini mlipata fursa ya  kudhihirishiana kuwa kweli mnapendana na mapenzi yenu yanatoka mioyoni  mwenu.
Baada ya kusema hayo sasa nirudi katika kile nilichodhamiria  kukiandika wiki hii. Nazungumzia tabia ya baadhi ya wake za watu hasa  wale wanaoishi nyumba za kupanga kujiweka katika mazingira ya  kuzibughudhi ndoa zao.
Matukio ya flani kutembea na mke wa mpangaji  mwenzake yamekuwa yakisikika mara kwa mara na ukijaribu kufuatilia  utabaini kuwa, wapo wanaume ambao wamekuwa wakijikuta wanawatokea wake  za watu kutokana na vishawishi wanavyopata.
Siyo kwamba nafagilia  wanaume wanaowatokea wake wa wenzao kwa kuwa tu wamepata vichocheo,  hapana! Nazungumzia hizi tabia mbaya wanazokuwa nazo baadhi ya wanawake  za kuwatega wenzao kwa mavazi, kwa makusudi au bila kujua.
Kuna hili  vazi la khanga moja ambalo baadhi ya wanawake hupendelea kulivaa hasa  wanapokuwa chumbani na wapenzi wao. Kulivaa huko ni sahihi kabisa kwani  unapokuwa na mtu wako faragha huchaguliwi cha kuvaa, hata usipovaa  chochote sawa tu lakini ishu ni pale unapokuwa nje ya chumba au nyumba  unayoishi.
Wapo wake za watu ambao ni wa ajabu sana na hili  nitalizungumza kwa kurejea tukio moja lilitokea juzikati maeneo ya  Sinza, Dar. Kuna mama mmoja anaitwa mama Frank, yeye amejaaliwa kuwa na  makalio makubwa.
Mama huyo ameolewa na mume wake anajiheshimu sana  lakini kitu ambacho wamekuwa wakikorofishana mara kwa mara ni tabia ya  mwanamke huyu kupenda kuvaa nguo za kihasara.
Mara kavaa taiti na  kitopu kisha anatulia kibarazani, mara kavaa khanga moja kisha anakatiza  kwenye korido kwa staili ya ‘hamsini… hamsini… mia…’ yaani kwa raha  zake.
Juzikati saa tatu usiku mama huyo alitoka akiwa na khanga moja kwenda kuoga bafu la nje ambalo liko mbali kidogo.
Wakati  anatoka mlangoni, mwanamke huyo akakutana na kijana wa kiume mlevi,  naye alikuwa anaelekea chooni. Yule kijana kutokana na jinsi yule mama  alivyokuwa akitingisha, uvumilivu ukamshinda, akamvaa na kutaka kumbaka.  Majirani ndiyo waliozuia tukio hilo la ubakaji lakini baadhi ya  wapangaji walimsema mtu mzima huyo kutokana na staili yake ya uvaaji.
Ninachotaka  kukisema kupitia tukio hilo ni kwamba, mke wa mtu hasa wewe unayeishi  nyumba ya kupanga huna sababu ya kuvaa khanga moja unapokuwa nje ya  chumba chako unacholala. Hata ‘sitting room’ siyo sahihi kabisa labda  kama umekaa na mumeo na mlango umefungwa.
Nasema hivyo kwa kuwa,  kuvaa hivyo kunakufanya utafsiriwe tofauti. Hebu jiulize kuna sababu  gani ya kuwaonesha wanaume wengine jinsi ulivyoumbika? Ili iweje sasa?  Wakutongoze halafu iweje?
Jamani kujiheshimu ni pamoja na kuchagua  unavaa nini ukiwa wapi. Kitendo cha wewe kwenda kuoga bafu la nje ukiwa  umevaa kanga moja na kukatiza mbele za wanaume kwanza unaonesha  kutokujijali lakini pia unajiweka katika mazingira mazuri ya kubakwa.
Ndugu  zangu leo nilitaka kulizungumzia hilo, ni kwa kifupi lakini naamini  utakuwa umenielewa na kulifanyia kazi ili uweze kuishi maisha yasiyo na  migogoro.
Saturday, March 17, 2012
Khanga moja nyumba ya kupanga? Unaitaka ndoa yako?
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment