WIKI hii tunamalizia mada yetu ambayo huwa tunaeleza mambo ambayo yatasaidia kutuwezesha kuishi kwa mafanikio na furaha zaidi.
Nakuomba uendelee kutafakari kila dondoo ambazo nitaziandika hapa chini kwa ufupi sana kama ifuatavyo:
Usijihangaishe  na jinsi watu wanavyokufikiria : Usitake maoni ya watu wengine  yakakuzuia kufanya jambo fulani, utayatia maanani tu pale unapotaka  kujitokeza kwa kishindo kama vile kwenye usaili, kukutana na mtu  mwingine kwa mara ya kwanza, na kadhalika.  Mambo ambayo watu  huyafikiria na kuyasema kuhusu wewe si muhimu.  Muhimu ni vile ambavyo  wewe mwenyewe unajihisi.
Acha nia ya kutaka kudhibiti kila kitu:  Maisha ni muujiza usiotabirika.  Hali inaweza kuwa nzuri au mbaya leo,  lakini hatuwezi kufahamu kwa asilimia 100 hali hiyo itakuwaje baadaye.   Hivyo itumie vyema zaidi fursa iliyo mbele yako na mengine mwachie  Mungu.
Acha kufanya kitu kilekile kila mara: Ili kukua ni lazima  upanue uwezo wako wa kuona mbali na kujiondoa katika mazingira ya  raha.    Ukiendelea kufanya kitu kilekile, basi utaendelea kuvuna  hichohicho ambacho unakivuna kila siku.
Usikubali kufuata njia ya  kutatua mambo kirahisi:   Maisha si rahisi hususani unapotaka kupata  mafanikio makubwa na yenye thamani.  Usitake kukimbilia ufumbuzi wa  haraka wa matatizo.  Fanya kitu ambacho si cha kawaida, yaani kile  ambacho hujawahi kukifanya.
Usitake kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja:  Fanya kila jambo kwa wakati wake  na hakikisha unalifanya vyema.
Acha  kufikiri kwamba watu wengine wana bahati kuliko wewe: Fahamu kwamba  ukifanya kazi kwa nguvu zaidi, ndivyo utakavyokuwa na bahati zaidi.
Usijibebeshe  majukumu mengi mno:  Ni vyema mtu  kuwa peke yako  na ni vyema wakati  mwingine kutofanya jambo lolote.  Hivyo, utumie muda wako kwa kutafakari  mambo mbalimbali na  kupumzisha mwili na akili.
Acha kufanya maamuzi  ya kukurupuka: Usikubali busara yako ikavurugwa kwa kufanya mambo kwa  kukurupuka.  Tulia na tafakari mambo yote kabla ya kufanya uamuzi ambao  utaleta mabadiliko katika maisha yako.
Usifanya makosa kwa  makusudi kwa vile hayatakuletea madhara: Usifanye jambo lolote makusudi  kwa vile tu halitakuletea madhara yoyote.  Fikiria mambo yote kwa mapana  zaidi  na ufahamu mwisho wake utakuwaje.  Fanya kile ambacho moyoni  unaamini ni kitu sahihi.
Usilifikirie kabisa jambo ambalo hutaki  likutokee: Elekeza mategemeo yako katika mambo ambayo unataka  yakutokee.    Fikra njema ndiyo silaha ya mafanikio yote makubwa.     Ukiamka kila asubuhi na fikra kwamba kitu fulani kizuri kitakutokea  maishani mwako leo  na ukakiwekea maanani, utakuja kugundua kila mara  kwamba fikra hizo ni sahihi.
Acha kujiona umebanwa na majukumu  kila siku: Kuna watu wachache hupenda kujiona wana majukumu kila siku.   Hata hivyo, jaribu kufurahia maisha na kupata burudani kila unapoweza.
Acha  kuyapitisha maisha yako ukifanya kazi ambayo huipendi: Ukifanya kazi  ambayo huipendi ni lazima maisha yatakuwa mafupi sana kwako.  Chaguo la  kazi sahihi hutegemea jambo moja; Kupata na kuifanya kazi ngumu ambayo  unaipenda.  Hivyo, ukijikuta unafanya kazi nzito lakini unaipenda, basi  endelea nayo.  Ukifanya hivyo, utakuwa unaelekea kwenye neema, kwani  kazi ngumu inakuwa si ngumu kama unaipenda.
Usifikirie vitu  ambavyo huna: Kubaliana na kitu chochote ambacho unacho, kwani watu  wengi huwa hawana bahati ya kupata vitu wanavyovipenda.
Mwisho.
Thursday, March 15, 2012
Mambo ya muhimu ya kuzingatia kwenye maisha ya kila siku III
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment