Thursday, March 15, 2012

Mambo ya muhimu ya kuzingatia kwenye maisha ya kila siku I

WIKI hii kwenye makala haya ya Jitambue tutajifunza mambo muhimu ambayo yatasaidia kutuwezesha kuishi kwa mafanikio na furaha zaidi. Ombi langu kwako msomaji ni kutafakari kwa kina dondoo zifuatazo ambazo nitazifasiri kwa ufupi sana.

Usiwe mtumwa wa umakini sana – Watu wengi hawafanikiwi kwa sababu ni watumwa wa umakini, hawafanyi au hawajaribu kufanya mambo ambayo akili zao zinawasiwasi nayo. Usiwe mtumwa wa usahihi, dunia haiwasifii wale wanaofanya mambo kikamilifu, bali huwasifia wale ambao hujitahidi kufanya chochote na kufanikiwa.

Usitake kujilinganisha na wengine – Fahamu kwamba katika kila ulifanyalo, mtu unayeshindana naye ni wewe mwenyewe.
Usifikirie sana mambo yaliyopita au kuhangaikia sana mambo ya siku zijazo – Fikiria na kujishughulisha na mambo yaliyopo sasa. Wakati huu ndiyo wa maisha yako yanayofahamika. Usiikose fursa hii.

Acha kulalamika – Dawa ya kulalamika ni kufanya kitu fulani ili kulitatua tatizo linalokukabili.
Usiwe na moyo wa kuendeleza kinyongo – Kuendeleza moyo wa kinyongo ni kupoteza muda ambao ungekufanya uwe na furaha.
Usiwe mtu wa kusubiri kufanya jambo fulani baadaye – Kile ambacho hutakianza leo ni dhahiri hautakimaliza kesho. Maarifa na busara ni vya bure iwapo mtu atachukua hatua ya kufanya vitendo vinavyotakiwa.

Acha kusema uongo – Katika kila hali ukweli baadaye hujitokeza. Hivyo, inabidi uwe mkweli katika vitendo vyako, la sivyo hatimaye vitendo hivyo vitakuumbua.

Acha tabia ya kukwepa kufanya makosa – Kosa pekee ambalo litakuumiza ni kuamua kutofanya chochote kwa vile unaogopa mno kufanya kosa. Siku zote tunajifunza kutokana na makosa.
Acha kusema, “siwezi” – Kama Henry Ford alivyowahi kusema, “Ukifikiri unaweza au ukifikiri huwezi, bado uko sahihi.” Ukisema huwezi hutaweza na ukisema naweza utaweza.

Acha kujiona unajua kila kitu na huna shida na watu wengine – Wakati mwingine maisha ya mwanadamu yanategemea mawazo ya wenzake, kuwa tayari kujifunza kutoka kwa wengine.
Acha kufikiri kwamba hauko tayari kufanya jambo fulani – Kuwaza mafanikio ni kujiumiza, mara kadhaa unapofikiria kufanya jambo fulani utaona kama haliwezekani na hali ya kufadhaika hutokea, jiamini usiwe mtu wa kukata tamaa.

Acha kujiwekea malengo madogo – Watu wengi hujiwekea malengo madogo kwa vile huwa wanaogopa kushindwa kuyatekeleza. Ukweli ni kwamba, kujiwekea malengo madogo ndiko kunakowafanya washindwe katika maisha. Weka malengo makubwa ya mafanikio ili ukipata kidogo usiwe kwenye fungu la kukosa.

Usitake kila kitu ukifanye wewe – Wewe ni sehemu ya watu wengine ambao unaishi nao kwa muda mrefu zaidi. Mkifanya kazi pamoja mtakuwa na nguvu zaidi kuliko ambavyo ungefanya jambo fulani pake yako.
Acha kununua vitu ambavyo huvihitaji – Hakikisha unazitumia fedha zako kwa busara na usikubali zikakutawala. Usitake kuzitumia kwa mambo ya kuwafurahisha wengine. Usitake kuwa na maisha ya kujipumbaza kwamba utajiri hupimwa kwa vitu ambavyo mtu anavyo.

Acha kuwalaumu watu wengine kwa matatizo yako – Kiwango cha kutimiza ndoto maishani mwako kinategemea jinsi unavyoyashughulikia maisha yako. Ukianza kuwalaumu wengine kwa yale yanayokutokea, utakuwa unajivua majukumu, kwani majukumu ya kutatua matatizo yako unakuwa umewapa watu wengine.
Itaendelea wiki ijayo.

Related Posts by Categories



No comments:

Post a Comment