Saturday, March 17, 2012

Sheria za kuwa maarufu,mwenye mamlaka na ushawishi katika jamii

Hakikisha ujuzi wako haumfuniki mkuu wako au watu wengine

Unaweza isiwe ujuzi pekee, lakini hata uwezo wako wa kiakili, mali na uelewa. Hakikisha hauutumii kwa majivuno kuonesha jinsi unavyowazidi wenzako kazini, kwenye biashara, darasani hasa watu waliokuzidi cheo. Siku zote hakikisha kuwa, unawatanguliza wenzako, kuthamini mchango wao na kusifu uwezo wao.

Kizuizi kikubwa kabisa kwenye maisha ya umaarufu, heshima na mamlaka kwenye jamii ni kujiona bora kuliko wenzake, jambo linalowafanya watu pamoja na uwezo wao washinde kuheshimika na kupendwa.

Usiwaamini mno marafiki, jifunze kuwatumia maadui zako

Jihadhari na marafiki, kwani wanaweza kukusaliti haraka zaidi maana ni rahisi sana wao kukuonea wivu. Watu hao wanaweza kubadilika na kuwa wakatili. Ukianzisha uhusiano na mtu ambaye aliwahi kuwa adui yako utagundua kwamba atakuwa mwaminifu zaidi kuliko rafiki, kwa vile atataka kukuthibitishia kwamba uhusiano wenu ni wa dhati. Kwa kifupi, waogope zaidi marafiki zako kuliko maadui.

Katika safari ya kuelekea kwenye kilele cha umaarufu na heshima, kuwa na maadui ni jambo muhimu kwani husaidia kuongeza ari na huthibitisha uwezo wako hasa pale inapotokea maadui hao wamesalimu amri kwako.

Dhamira zako zifanye siri

Hakikisha watu hawakuelewi kwa dhamira zako au sababu ya kile unachokifanya. Kama hawafahamu nini unataka kukifanya, ni dhahiri watakuwa hawana nguvu ya kukufanya lolote. Hakikisha unawapotosha wasijue mipango yako na wakati watakapofahamu dhamira yako, watakuwa wamechelewa kwani utakuwa tayari umeikamilisha.

Epuka kuwa mtu wa kuropoka juu ya madhumuni yako ya maisha, utawapa nafasi wabaya wako kukuwekea vikwazo vya kukuzuia usifike mahali ulipokusudia.

Usipende kuzungumza sana

Unapotaka kuwavutia watu punguza wingi wa maneno yako, kusema sana kunaweza kuwafanya wanaokusikiliza wakukinai. Watu maarufu huweza kuwavutia na kuwaogopesha watu kwa kusema maneno machache. Jinsi unavyozungumza zaidi, ndivyo unapojenga uwezekano wa kusema kitu cha kipumbavu kitakachokufanya udharauliwe.

Hakikisha unalinda hadhi yao katika jamii

Hadhi katika jamii ndiyo nguzo ya mamlaka.Kwa kutumia hadhi yako pekee unaweza kuwaogopesha wengine na ukafanikiwa mambo yako, lakini ukipotoka tu, fahamu umeingia matatani na utashambuliwa kutoka pande zote. Hakikisha hadhi yao inabaki imara.

Kila mara jihadhari na mashambulio yanayoweza kutengenezwa kwa lengo la kukuondolea heshima, kuwa mjanja kujitetea kwa hoja na pita njia ya nyuma kuwavurugia wanaotaka kukuangamiza. Epuka kuwahukumu adui zako, acha wahukumiwe na jamii inayokuunga mkono.

Hakikisha jamii inakutambua

Kila kitu huamliwa kutokana na mwonekano wake, kisichoonekana hakina maana yoyote. Usikubali jamii isikutambue kiasi cha kusahaulika kama upo. Jitokeze mbele. Jionyeshe kwa watu katika namna yoyote, iwe ya kusaidia au kushirikiana na wenzako katika shida na raha. Jifanye kivutio katika jamii kwa kujitokeza zaidi, kujijengea umaarufu kuliko watu wengine.


Waache watu wakufanyie kazi kwani sifa utapata wewe

Kuwa mjanja, hakikisha unatumia busara na ujuzi wa watu wengine katika kuendeleza masilahi yako. Msaada huu hautaokoa muda na nguvu zako tu, bali utakupa umaarufu wa kufanya kazi vyema na kwa kasi. Mwisho wa yote, watu wanaokusaidia watasahauliwa na badala yake ni wewe utakayekumbukwa.

Kama wewe ni mwanasiasa kwa mfano, usifanye kila kitu wewe, tafuta watu wenye ushawishi kwenye jamii zao, watume wafanye utakayo, mwisho wa siku ushindi utakuwa wako.

Wafanye watu wakufuate kwa kuweka vivutio

Ukimlazimisha mtu mwingine kufanya kitu, ujue wewe ndiye mshika usukani. Siku zote ni vyema zaidi kumleta mpinzani wako kwako, jambo ambalo litamfanya aiache mipango yake yote. Mvutie kwa kumwonyesha mafanikio yako makubwa, kisha mmalize, kwani wakati huo wewe utakuwa umeshika mpini wa kisu.

Daima, hakikisha kuwa mafanikio yako yanakusaidia kuvuta watu kwa namna yoyote, iwe ya kusaidia, kununua siri, kutoa motisha na hata kuwachonganisha wanaokuchukukia ili washuke na wewe upate nafasi ya kung’ara zaidi kwenye jamii.

Shinda kwa vitendo, si kwa maneno

Ushindi wowote wa muda mfupi unaotokana na maneno ni ushindi bandia. Chuki na nia mbaya unazoweza kuziibua zina nguvu zaidi na hudumu zaidi kuliko mabadiliko ya muda ya maoni fulani. Ni rahisi zaidi kwa watu wengine kukubaliana nawe kwa kuonyesha vitendo bila hata kusema chochote. Onyesha kwa mifano si kwa maneno mengi.

Waepuke watu wasio na furaha, wasio na bahati

Unaweza kufa kutokana na matatizo ya mtu mwingine, kwani hali ya mtu mwingine inaambukiza kama ugonjwa. Unaweza kuhisi unamsaidia mtu aliye matatizoni, kumbe unajipalia matatizo na balaa. Fanya uhusiano na watu wenye furaha na wenye bahati siyo wenye mikosi na matatizo yasiyokwisha.

Jifunze kuwafanya watu wakutegemee

Ili kuendelea kujitegemea lazima kuwe na watu wanaokuhitaji kwenye maisha yao. Kumbuka watu wanavyozidi kukutegemea, ndivyo unavyozidi kuwa huru zaidi. Wafanye watu wakutegemee ili waweze kupata furaha na ustawi usiogope wala usizuie watu tegemezi.
Ukitaka kuwa maarufu usikubali kuwafanya wenzako waweze kuishi bila wewe. Epuka kuwapa mbinu za kujitegemea kwani wakifanikiwa utapoteza umaarufu kwao na bila shaka watakudharau.

Chagua wema na ukarimu utakaowavunja nguvu maadui zako

Jambo moja jema hufukia mabaya mengi yaliyofanywa na mtu. Wema na ukarimu unaofanywa kwa moyo mkunjufu humvutia hata mtu aliyekuwa na wasiwasi na wewe.
Wema huo uliopangwa unapowavutia watu, ni wazi unaweza kuwalaghai na kuwatumia jinsi utakavyo. Zawadi yoyote inayotolewa kwa muda unaotakiwa inaweza kufanikisha lengo lako la kumtumia umtakaye kwa faida yako.

Epuka kukumbusha wema wako mbele ya jamii, acha kuutumia wakati wa kuomba msaada.
Unapotafuta msaada kutoka kwa rafiki, usitake kumkumbusha misaada au vitendo vyema ulivyomfanyia. Ukimwambia hivyo anaweza akakupuuza, badala yake mweleze kitu kipya katika kuomba msaada huo au katika uhusiano wenu, kitu ambacho kitamnufaisha. Kisisitize kitu hicho kwake.

Atakusaidia kwa furaha mara atakapoona kuna kitu ambacho naye kitamnufaisha.
Jifanye rafiki wa mpinzani wako, lakini fanya kazi naye kama jasusi.
Ni muhimu kumfahamu vyema mpinzani wako, ufahamu huo utaupata pale utakapoamua kuwa rafiki wa adui yao na kutumia ukaribu huo kuchunguza mbinu zake ili baadaye umshinde kwa udhaifu wake utakaoujua.

MWANGAMIZE KABISA ADUI YAKO

VIONGOZI wote maarufu tangu Musa wamefahamu kwamba adui anayeogopewa ni lazima aangamizwe kabisa. (Wakati fulani wamelitambua hilo kwa matatizo.) Iwapo ukuni mmoja ukiachwa unawaka, hata kama una moto mdogo kiasi gani, hatimaye moto utalipuka. Mambo mengi hupotea kwa kufanywa nusu nusu badala ya kuyamaliza kabisa: Kumwacha adui yako akinusurika kunaweza kuleta kisasi kitakachokugharimu maisha.

KUTOONEKANA SANA KUNAONGEZA HESHIMA
Kuonekana mno kunapunguza thamani ya mtu: Unapoonekana mara kwa mara na kusikika kila mara, ndivyo unavyozidi kuonekana mtu wa kawaida. Ikiwa umejijenga katika kundi fulani, jiondoe kwa muda, jambo ambalo litakufanya uzungumziwe zaidi na kupendwa zaidi. Jifunze ni wakati gani wa kujitokeza hadharani. Unapoadimika ndivyo unavyokuwa na thamani mbele za watu.

WAFANYE WENGINE WAISHI KATIKA WOGA
Binadamu ni viumbe wanaopenda kufahamu mambo ya wengine. Wakikufahamu kwa undani wanaweza kukutawala. Wachanganye: Uwe mtu usiyetabirika. Tabia isiyofahamika itawafanya washindwe kukuzoea na hivyo kujenga hofu kwako: “Mmmm…huwa hatabiriki unaweza kusema hatajali akaja kukuadhibu.”

USITAKE KUJITENGA KWANI NI HATARI
Dunia ni ya hatari na maadui wako kila mahali, kila mtu inabidi kujilinda. Kujitenga kunaonekana kuwa ndiyo njia salama zaidi. Lakini kujitenga kunakuweka katika hatari zaidi kuliko kukulinda. Kunakunyima fursa ya kupata habari muhimu. Ni vyema kuchanganyika na watu na kupata marafiki. Uhusiano na watu wengine ni kinga ya maadui zako.

MFAHAMU MTU UNAYESHUGHULIKA NAYE
Kuna watu wa aina nyingi duniani na huwezi kudhani kwamba kila mmoja atakabiliana nawe katika namna ile ile. Walaghai na kuwachanganya baadhi ya watu ili ikitokea uadui au hali ya kutotaka kukuunga mkono wao kwa wao waanze kupingana. Ni muhimu kuwafahamu waliokaribu nawe.

USITAKE KUJIUNGA NA UPANDE WOWOTE
Mpumbavu huharakisha kujiunga na upande fulani. Usitaka kujiunga na upande wo wote au suala fulani bali tumikia nafsi yako. Ukiendelea kuwa mtu huru, utakuwa ni bwana wa watu wengine, ukiwagonganisha watu na kuwafanya wafuate utashi wako. Kama uko mtaani usikubali kuwa mwanachama wa makundi hasimu.

JIFANYE MNYONGE: UBADILI UNYONGE WAKO KUWA NGUVU.
Ukiwa mnyonge, kamwe usijaribu kupigana; badala yake jifanye umesalimu amri. Kusalimu amri kunakupa muda wa kujipanga upya, muda wa kumchanganya na kumkasirisha adui yako, muda wa kusubiri hadi nguvu zake ziishe. Usitake kumpa heshima ya kupigana halafu akakushinda. Wewe salimu amri tu. Ukifanya hivyo utamuudhi na kumfanya achanganyikiwe.
Lichukulie suala la kusalimu amri kama chombo cha kukupatia nguvu.

IMARISHA NGUVU ZAKO
Imarisha nguvu na juhudi zako kwa kuhakikisha ziko katika hali ya juu. Siku zote nguvu zinazokwenda sehemu moja hushinda zaidi ya zile zinazogawanywa mara nyingi.

Wachagulie watu kitu kitakachokunufaisha
Ulaghai mzuri zaidi ni ule unaoonekana kuwapa watu wengine chaguo la jambo la kufanya. Maadui zako watahisi wako huru kumbe ni vikaragosi wako.Wape watu chaguo ambalo litakunufaisha.Walazimishe wachague kitu ambacho kitakupa faida.Waweke katika hali ambayo watashindwa kujitoa bali waendelee kukunufaisha.

Jione mfalme na watu wakuone hivyo
Jinsi unavyojiona ndivyo watu watakavyokuchukulia pia. Ukijipa mwonekano wa ovyo watu watakuona mtu wa ovyo na kutokuheshimu. Mfalme hujiheshimu na huwafanya wengine kuwa na hisia hizo pia. Kwa kufanya mambo kama mfalme na kujiamini ni dhahiri unajipalilia njia ya kuvishwa taji la mafanikio.

Jua kuutumia muda wako
Kamwe usitake kuonekana una haraka, kuharakisha mambo kunakufanya ushindwe kujidhibiti na kuudhibiti muda. Siku zote onekana huna haraka, kama vile unajua kila kitu kitakamilika. Ufahamu wakati muafaka wa kufanya jambo, fahamu nguvu ya muda na njia ambazo zitakuletea mafanikio. Jifunze kusubiri wakati muda haujafika na kuutumia ipasavyo wakati unapowadia.

Chukia vitu ambavyo hutavipata, vidharau
Kukubali tatizo dogo likukere ni kulikuza na kulifanya liaminike. Unavyozidi kumfikiria adui yako ndivyo unavyomfanya awe na nguvu zaidi. Tatizo dogo huwa kubwa zaidi na lenye kuonekana zaidi unapojaribu kulitatua. Wakati mwingine ni kuyaacha mambo kama yalivyo. Kama kuna kitu unakitaka na huwezi kukipata, kidharau. Unavyokipuuza ndivyo unavyozidi kujipunguzia matatizo.

Fikiri unavyotaka lakini ishi kama wengine
Ukionekana kwenda kinyume na nyakati, ukaacha tabia na mazoea yako ya siku zote, watu watafikiri unataka kuvutia nadhari yao na kwamba unawadharau. Watatafuta njia ya kukuadhibu kwa kuwafanya waonekane si lolote kwako. Ni vyema kuendelea na tabia yako ya siku zote. Endeleza tabia yako halisi na marafiki zako.

Mchokoze adui ili umfahamu undani wake
Chuki na munkari huzaa hasara. Ni lazima uwe mtulivu na mwenye busara. Lakini ukiweza kumuudhi adui yako na ukabaki umetulia, jambo hili linaweza kukuletea faida. Mchokoze adui yako kwa kumuudhi ili uweze kumtambua alivyo.

Kataa vitu vya bure
Vitu vinavyotolewa bure huwa ni vya hatari, kwani hujumuisha njama fulani au malengo yaliyojificha. Kilicho na thamani basi kigharamie. Kwa kununua kitu utakuwa umejipa furaha, ukakwepa kujiona una deni au kulaghaiwa. Ni vyema kitu ukakinunua. Tumia fedha zako kikamilifu kwani ukarimu ni sumaku inayovuta nguvu.

Epuka kutumia mafanikio ya waliokutangulia
Kinachotokea kwanza siku zote huonekana chema zaidi na chenye asili zaidi kuliko kinachofuata. Ukimrithi mtu maarufu au mzazi maarufu, utalazimika kupata mafanikio mara mbili zaidi kuliko yao. Usipotelee katika vivuli vyao bila ya wewe kufanya lolote. Jenga jina lako na utambulisho wako kwa kubadili mwelekeo. Yafute majina ya waliokutangulia kwa kujenga nguvu yako mwenyewe.

Related Posts by Categories



No comments:

Post a Comment